Saturday 14 May 2016

HATUA 11 KUELEKEA UJASIRIAMALI WENYE MAFANIKIO


Imeandikwa katika Historia kuwa, wafanyabiashara wakubwa katika zama zilizopita hasa kwenye ukanda wa Mashariki ya kati ya dunia (Middle East) walikuwa ni Waislamu. Wao walizifanya shughuli zao za kiujasriamali kama Ibada na ni moja ya njia za kueneza dini na kutengeneza jamii yenye tabia njema iliyojaa uaminifu na uadilifu pia. Waliweza kufikia kilele cha juu kabisa cha maadili katika shughuli zao. Kwa ufupi tunaweza kusema, walikuwa ni wajasiriamali waliofanikiwa (Duniani na Akehra) jambo ambalo wajasiriamali wa karne hii ya 21 wamelipoteza

Zifuatazo ni hatua 11 za kuelea Ujasiriamlai wenye Mafanikio.

1.      Kuwa na Ikhalas.

Imesemwa katika Hadithi kuwa Matendo hulipwa kutokana na nia na kila mtu atalipwa matendo yake kulingana na nia aliyoiweka kwenye matendo hayo. Ifanye Biashara yako kama ni moja ya sehemu ya kupata Radhi za Mwenyezi Mungu. Kuwa na Ikhlas ndani yake na uifanye kwa kutegemea kuwa Allah atakulipa malipo yaliyo ya kheri kutokana na biashara hiyo.

2.      Fanya Istikhara.
Istikhara ni kumuomba Mwenyezi Mungu ushauri na ukupe maamuzi yaliyo na kheri nawe kwenye jambo linalokutatiza. Allah ndiye nayetujua zaidi kuliko tunavyojiujua sisi wenyewe. Ni vizuri kufanya Istikhara kabla ya kuanza biashara zetu na kumuomba Allah akupe yaliyo na kheri kwenye biashara yako hiyo. Jifunze Jinsi ya Kuswali swala ya istikhara hapa.

3.      Fanya Shura.

Mwenyezi Mungu amewasifu waumini kwa sifa ya kufanya majambo yao na kuyapeleka kwa mfumo wa “Shura” (42:38). Shura ni kutafuta ushauri na maoni juu ya jambo Fulani kutoka kwa watu wengine. Ni vizuri ukapata ushauri juu ya Biashara yako kutoka kwa wataalamu waliobobea na wenye kuaminika kulingana na bishara uliyonayo.

4.      Jielimishe.
Moja kati ya Sifa za Mjasiriamali wa Kiislamu ni kupenda kujielimisha. Kujielimisha huku kunatakiwa kuanzie mwanzoni na kuendelea nako kwenye mchakato mzima wa kuelekea bishara yenye mafanikio. Jielimishe kupitia Vitabu sahihi vinavyohusu Biashara yako, hudhuria semina na ikiwezekana jiunge na kozi mbalimbali zitakazokusaidia kuwa madhubuti kwenye Biashara yako.

5.      Angalia Mtaji Wako.

Moja kati ya maswali ya kujiuliza mjasiriamali akiwa kwenye mchakato wa kuanzisha biashara ni mtaji wake. Ni lazima ajue anahitaji kiasi gani cha mtaji na wapi atapata mtaji huo. Ni vizuri kwa mjasiriamali wa kiislamu ahakikishe biashara yake inaanzishwa na mtaji wa halali na anaouridhia Mwenyezi Mungu. Pia ni lazima aanzishe biashara inayoendana na mtaji wake na achunge mtaji huo usije ukapotea kizembezembe.

6.      Angalia Fursa Zilizopo.

Usije kuanzisha Biashara ambayo sio Fursa kwani huenda ukakosa muendelezo mzuri wa biashara hiyo. Ni lazima uangalie Fursa zilizopo ndani ya biashara unayotaka kuanzisha na hata nje ya biashara yako hiyo. Angalia fur’sa za halali na zenye kuleta tija katika jamii inayokuzunguka.

7.      Weka Ratiba Madhubuti.

Si katika maisha ya kila siku tu, hata kwenye masuala ya ujasiriamali, suala la ratiba lina umuhimu mkubwa sana. Sio Ratiba tu ilimradi ratiba, ila ni ratiba madhubuti. Hakikisha unaandaa ratiba nzuri ya shughuli zako kwa kuzingatia masuala ya kiibada, kijamii, kiafya n.k

8.      Simamia Malengo Yako.

Mafanikio ya kwenye maisha yako ya duniani na akhera yapo kwenye mikono yako mwenyewe. Ukiwa kama mjasiriamali wa kiislamu ni lazima uhakikishe unasimamia malengo yako uliyojiwekea. Usikubali kuyumbishwa (bila sababu ya msingi). Kila siku kabla ya kulala ni lazima ujifanyie hesabu ni kwa kiasi gani umeyafikia malengo uliyoyakusudia, na kila unapoamka lazima ujiwekee njia utakazotumia kwa siku hiyo kuyafikia malengo hayo.

9.      Tengeneza Mtandao wenye Manufaa.

Hakuna jambo zuri kwenye maisha na kwenye ujasiriamali (hasa wa kiislamu) kama mtu kuwa na mtandao wenye manufaa. Hakikisha unazungukwa na watu ambao watakusaidia kwa namna moja ama nyingine kufikia malengo uliyoyakusudia. Hakikisha unakuwa na mawasiliano yao ya simu, barua pepe (email), na kujua sehemu zao za kazi na vipi wataweza kukusaidia kwenye kutimiza malengo yako.

10.  Jifunze Kutokana na Makosa.

Asilimia kubwa ya watu wasiojifunza kutokana na makosa (aidha waliyoyafanya wao au yaliyofanywa na wengine) huwa wana tabia ya kurudia makosa yaleyale. Kama mjasiriamali wa kiislamu ni lazima ujue ulipokosea na uweke mikakati madhubuti ya kutorudia tena makosa hayo.

11.  Safisha Mali Zako.

Naam usafi wa mali ni jambo la muhimu sana kwa mjasiriamali wa kiislamu. Jambo hili limesahaulika mno na wajasiriamali wengi wa kiislamu. Njia kuu ya kusafisha mali zako ni kwa Kutoka zaka (kama kiwango cha mali zako kinafikia kutoa zaka). Njia zingine ni kutoa sadaka, kusaidia wanafunzi malipo yao ya masomo, kusaidia masikini n.k

Kwa Muislamu, Ujasiriamali ni sehemu ya Ibada na ni moja ya njia zinazoweza kutumika kuufikisha uislamu katika ubora wake. Ni vizuri tukawa na malengo makubwa ya kufanya shughuli zetu za kiujasiriamali ni zenye kufanikiwa kwa kufuata kanuni na sheria zilizopo kwenye uislamu insha allah.

Maassalaam.

No comments:

Post a Comment