Friday 22 April 2016

MASWALI 20 YA KUJIULIZA KABLA YA KUANZISHA BIASHARA



Asilimia kubwa ya vijana wamekuwa kwenye moto wa kutaka kuanzisha Biashara zao wenyewe. Ila wengi wao hawajui (na wala hawazingatii) mambo muhimu ambayo mtu inabidi ayafanye kabla ya kuanzisha biashara.
Kuna maswali muhimu 20 ambayo Mjasiriamali aliyekuwa na Malengo ya Kufika mbali anapaswa kujiuliza kabla hajaanza kufanya Biashara yake.
Maswali hayo ni haya yafuatayo
1.      Kwa nini nataka kufanya Biashara?
Hili ndio swali la kwanza kujiuliza. Ni lazima ujue sababu kuu zinazokufanya utake kuanzisha Biashara. Usije ukaanzisha Biashara kwa sababu tu umemuona fulani kaanzisha basi nawe ukaanzisha. Wengi wamepoteza muelekeo wa Biashara zao kutokana na sababu kuwa walizianzisha Biashara hizo kwa sababu tu wameona wengine wameanzisha.
2.      Ni aina gani ya Biashara natakiwa kufanya?
Sio kila Biashara unayoiona inafanywa na wengine basi ukadhani kuwa nawe unaweza kuifanya. Ni lazima ujue ni aina gani ya biashara unaweza kuifanya kulingana na kiasi cha mtaji ulichonacho, taaluma, wafanyakazi n.k. Hivyo ni lazima ujiulize vizuri juu ya aina ya Biashara unayotakiwa kuifanya.
3.       Je Biashara hiyo ina wateja?
Dhumuni kuu la Uanzishwaji wa Biashara ni Kuuza ambapo mnunuzi ni Mteja. Hii ina maana kwamba kama Biashara unayoanzisha haitakuwa na wateja (wa kutosha) basi hutaweza kufanya vizuri kwenye Biashara hiyo. Hivyo ni vizuri mtu kuangalia kama Biashara yako unayotaka kuanzisha ina wateja wa kutosha au la.
4.      Ni bidhaa ipi au huduma gani itakuwa kuu kwenye Biashara yangu?
Ni lazima ujue ni Bidhaa ipi (au hutuma gani) itabeba biashara yangu. Mfano mfugaji wa kuku wa nyama, bidhaa yake kuu ni kuku mwenyewe ingawa anaweza kuuza Mbolea inayotokana na kinyesi cha kuku. Hivyo ni muhimu ujue kipi kitabeba Biashara yako.
5.      Nina muda wa kutosha kusimamia Biashara hiyo?
Biashara yoyote inahitaji muda wa usimamizi na ufuatiliaji. Wengi wamekuwa wakifeli kwenye biashara zao kutokana na kuanzisha Biashara halafu kuwaachia wengine wawaangalizie huku wao wenyewe wakiwa aidha na muda mchache au kutokuwa na muda wa kufuatilia maendeleo ya biashara zao. Hivyo ni vizuri kujiuliza kama utakuwa na muda wa kutosha wa kufuatilia Biashara hiyo unayotaka kuanzisha.
6.      Kipi kitakachotofautisha Biashara yako na Biashara zingine?
Biashara inahitaji ubunifu na upekee katika uanzishwaji wake. Kwenye Biashara unayotaka kuianzisha hautakuwa peke yako. Ni lazima watakuwepo watu wengine wanaofanya biashara hiyo. Hivyo ni lazima ujiulize ikiwa utaanzisha biashara hiyo, ni vitu gani vitakavyoweza kutofautisha Biashara yako na Biashara za watu wengine.
7.      Ni sehemu gani nzuri ya Kuiweka Biashara hiyo?
Location! Location! Location! (Sehemu! Sehemu! Sehemu!) ndio maneno yanayopendwa kutumiwa (kwa kurudiwa mara tatu) na wataalamu na washauri wa masuala ya kibiashara kuonyesha umuhimu wa sehemu ya kufanyia Biashara. Ni lazima ujue sehemu nzuri ambayo itaweza kufikiwa kwa urahisi na wateja ya kuweka Biashara yako. Pia ni vizuri kuangalia sehemu ambayo inafikiwa na huduma za kijamii kama vile maji, umeme, n.k. Uteuzi mbovu wa sehemu ya kufanyia biashara unaweza kufanya Biashara yako iwe ni yenye kuleta hasara na kushindwa kuendelea Daima. 
8.      Nahitaji wafanya kazi wangapi kwenye Biashara yangu?
Hili linategemea na ukubwa wa biashara. Sio Biashara zote zitahitaji wafanyakazi. Zipo nyingine zitahitaji uwepo wako tu. Hivyo kama biashara yako itahitaji wafanyakazi, ni vizuri kujua ni wafanyakazi wangapi wanaohitajika. Hili litakusaidia kuweka vizuri bajeti yako uanzishwaji wa Biashara.
9.      Kuna mfanyabiashara mwingine (Supplier) namuhitaji kwenye Biashara yangu?
Biashara huwa zinategemeana. Unaweza ukawa ni muuzaji na katika muda huo huo unaweza kuwa ni mnunuaji. Hivyo ni lazima ujue ni watu gani utakuwa unanunua vitu kwao ili kuendesha Biashara yako. Mfano Mkulima mbali na kuuza mazao ila pia atahitaji Pembejeo za kilimo, dawa n.k. kutoka kwa wafanyabishara wengine
10.  Ni kiasi gani cha pesa nahitaji ili Kuanza Biashara yangu?
Naam! Ni lazima uwe na kiasi cha pesa kitakachotumika kama mtaji wa kuanzia katika biashara yako (Start Up Capital). Hivyo baada ya kujua aina ya biashara unayotaka kufanya ni lazima pia ujue mtaji wake. Usianzishe Biashara ambayo inahitaji kiasi cha mtaji ambacho wewe huna au huwezi kukifikia. Wengi wamefeli kutokana na hili.
11.  Ni njia gani nzuri ya kutumia ili kupata Mtaji?
Zipo njia nyingi anazoweza kutumia mtu ili kupata mtaji wa biashara yake. Kujiwekea Akiba, kukusanya pesa kutoka kwa ndugu na marafiki, kukopa (Sio mkopo wenye Riba), kuwekeza faida (Retained earnings) ni miongoni mwa njia zinazoweza kutumika ili kupata mtaji. Hivyo ni muhimu na vizuri kujua njia utakazotumia ili kupata mtaji wa Biashara unayotaka kuanzisha.
12.  Itanichukua muda gani mpaka kukahakikisha Bidhaa yangu inawafikia wateja?
Hili ni swali ambalo wengi huwa hawajiulizi. Umuhimu wa swali hili ni kuwa litakusaidia kwenye kupanga matumizi mazuri kwenye Biashara yako. Unaweza ukakuta mtu anaanzisha biashara ambayo gharama za uendeshaji kwa mwezi ni Tshs 2,000,000 huku wateja aliowafikia hawafikishi hata mauzo ya Tshs 500,000. Huyu lazima atashindwa kuendelea na Biashara yake. Hivyo ni muhimu kujua muda utakaotumia kuwafikia wateja na kiasi utakachoingiza kwa muda huo.
13.  Itanichukua muda gani hadi kuanza kuiona faida ya Biashara yangu?
Lengo kuu la mtu kuanzisha Biashara ni kupata faida. Hivyo ni lazima ujue muda gani utatumika ili kuanza kupata faida tangu uanzishe Biashara hiyo. Hii itakusaidia kujua Uhai wa Biashara yako utakuwaje hapo mbeleni
14.  Ni nani wapinzani wangu kwenye Biashara?
Naam! Kama tulivyosema awali kuwa Huwezi kuwa peke yako kwenye Biashara unayoianzisha. Hivyo ni lazima uwajue wapinzani wako na mbinu wanazozitumia kwenye mauzo yao. Hii itakusaidia kubuni njia nzuri za kuendesha Biashara yako zitakazofanya uwashinde kwa wepesi.
15.  Ni kiasi gani cha bei au ubora wa bidhaa (au huduma) zangu nifanye ili kuwashinda wapinzani wangu?
Bei ya Bidhaa ni kitu muhimu cha kuzingatia kwenye uanzishwaji wa biashara. Sio lazima bei yako iwe chini ya wapinzani wako ndio uweze kuuza. Bei ya bidhaa huwa inawekwa kutokana na ubora wa bidhaa yako. Hivyo ni lazima uangalie bei na ubora ambavyo vitaweza kuwa vizuri kuliko wapinzani wako.
16.  Vipi nitafuata taratibu za kisheria kwenye Biashara yangu?
Kila biashara inayoendeshwa ina taratibu zake za kisheria kutokana na nchi na nchi. Hivyo ni lazima ujue taratibu za kisheria zinazohitajika kwenye biashara yako na uzifuate ipasavyo. Wengi wameshindwa kuendelea na biashara zao katika ubora wake kutokana na kushindwa kufuata taratibu za kisheria zilizopo kwenye bishara zao.
17.  Malipo ya kodi?
Kodi ni jambo la lazima katika Biashara. Hivyo ni lazima ujue ni kiasi gani kinahitajika ili kueweza kulipa kodi. Pia ujue ni taratibu gani za kufuata katika malipo yako hayo ya kodi.
18.  Matangazo?
"Biashara Matangazo." Ni msemo wa waswahili katika Biashara. Ni lazima ujiulize vipi utafanya matangazo ya Biashara yako. Ni lazima ujue njia gani zitatumika kuwafanya watu wajue biashara yako. Njia hizo ni vizuri zikawa na gharama nafuu na zenye kuleta Tija katika Biashara yako.
19.  Uongozi na Usimamizi?
Biashara inataka usimamizi mzuri na uongozi wa kuiendesha Biashara hiyo. Ni lazima wapatikane watu makini na wenye ari ya kutimiza majukumu yao. Ikiwa uongozi wa kwenye Biashara yako hautakuwa madhubuti na usimamizi usipokuwa wenye kueleweka, basi biashara hiyo lazima itafeli.
20.  Inaruhusiwa kwenye Uislamu?
Hili ni swali la msingi sana kwa mjasiriamali wa kiislamu. Ni lazima ujue kama Biashara yako inaruhusiwa au hairuhusiwi kufanywa kwa mujibu wa Uislamu. Unaweza kuomba ushauri kwa wataalamu wa masuala ya dini na wakakujibu juu ya uhalali na uharamu wa Biashara unayotaka kuanzisha.

HITIMISHO :
Usiwe na Pupa ya kuanzisha biashara bila ya kufanya utafiti wa kutosha juu ya biashara hiyo. Ni lazima utengeneza mpango mzuri wa biashara yako kama unahitaji biashara hiyo iwe ni yenye kukufikisha mbali Insha Allah.
Maassalaam.


No comments:

Post a Comment