Monday 16 May 2016

KIWANDA CHA SUKARI MANYARA CHATAKA MIWA ZAIDI



KIWANDA cha Sukari cha Manyara (Manyara Sugar) kilichopo katika kijiji cha Matufa wilayani Babati mkoani Manyara, kimeiomba Halmashauri ya Wilaya ya Babati kusaidia kuwaelimisha na kuwahamasisha wakulima kulima miwa kwa wingi kuongeza uzalishaji wa sukari nchini.
Meneja wa kiwanda hicho, Pratap Disodya aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa kiwanda hicho hakina sababu ya kuficha sukari kwa kuwa kina uwezo wa kuzalisha tani 300 hadi 500 kwa siku.
Alisema pamoja na uzalishaji huo unaochangiwa na upungufu wa miwa kutoka kwa wakulima, kiwanda hicho pia kinalazimika kufungwa kila mwaka ifikapo Desemba hadi Juni kusubiri uzalishaji uanze Juni.
Alisema katika kuitikia agizo la Rais John Magufuli la kuwataka wafanyabiashara wote walioficha sukari katika maghala yao kuanza kusambaza mara moja vinginevyo serikali itachukua hatua kali, kiwanda hicho kimethibitisha kutokuwa na akiba ya kutosha ya sukari inayozalishwa kiwandani hapo.
Alisema wakulima wakihimizwa kuzalisha miwa kwa wingi uzalishaji utaongezeka na kupunguza uhaba wa sukari nchini. Disodya alisema tangu kuanzishwa kwa kiwanda hicho mwaka 2005 na kuanza uzalishaji mwaka 2007, kimezalisha tani 150 mwaka 2013 pekee.
Alisema hatua walizochukua ni pamoja na uongozi wa kiwanda kuendelea kuwahamasisha wakulima wadogo zaidi ya 1,500 kuongeza uzalishaji wa miwa kwa kuwapatia mikopo.

Chanzo : Tovuti ya Habari Leo


No comments:

Post a Comment